AMCHINJA MKE WAKE GESTI NA KUMTOA MOYO NA MAINI



Huu ni ukatili namba moja kwa wanandoa duniani! Bado picha haijatoka kichwani kwa wakazi wa Manzese jijini Dar kufuatia kifo cha kuchinjwa cha  Josephine Ndengaleo Mushi kinachodaiwa kufanywa na mume wake wa ndoa, Remy Joseph (35).

Tukio hilo la kutisha kusimuliwa achilia mbali kuona, lilijiri saa 9: 10 alasiri ya Januari 29, mwaka huu ndani ya chumba kimoja kilichopo ghorofa ya pili ya  Hotel Friend’s Corner Ltd iliyopo Manzese Argentina, Dar.

Baada ya habari za mauji hayo kusambaa kama moto wa kifuu, waandishi wetu walianza kuichimba habari hii kwa kina.

Kwa mujibu wa mhudumu mmoja wa hoteli hiyo, Januari 28, mwaka huu, Remy na Josephine walifika kwenye hoteli hiyo na kuchukua chumba. Walionekana wenye amani, kwani hakuna sura iliyoonesha kuna tatizo.

“Walikuwa kama wateja wengine. Tena niliwauliza kama wanatoka mkoa, wakasema ni wakazi wa Dar es Salaam, wao ni mke na mume kwa ndoa, waliamua kulala hapa ili kuimarisha mapenzi yao, si lazima kila siku nyumbani,” alisema mhudumu mmoja.

Kwa mujibu wa baadhi ya wahudumu wa hoteli hiyo, siku ya pili, muda wa saa tisa alasiri, walishtuka kuona damu nyingi ikitoka ndani ya chumba walichopanga wawili hao.

“Tulishtuka sana. Tukajua kuna kitu kikubwa kimewapata. Ilibidi tuwagongee mlango ili tujue kilichowapata lakini mlango haukufunguliwa,” alisema mhudumu mwingine.

Kwa vile ukimya ulitawala ndani ya chumba hicho huku damu zikiendelea kutiririka, ilibidi uongozi wa hoteli hiyo yenye sifa ya ulinzi, uwasiliane na Kituo cha Polisi cha Ndugumbi ambacho kipo jirani.

Polisi walifika, wakagonga mlango kwa muda mrefu bila kufunguliwa mpaka baadaye sana ambapo mlango huo ulifunguliwa na mwanaume akiwa ameshika kisu mkono wake wa kuume.

Ndani ya chumba kulionekana damu zimetapakaa kila sehemu. Polisi walimsihi mwanaume huyo kuangusha kisu chini ili waongee lakini jamaa aligoma.

“Polisi walimwamuru mwanaume atupe kisu chini, akakataa. Sura yake wakati huo ilikosa mwonekano wa ubinadamu. Ndipo askari mmoja alitumia mbinu ya kivita, alimpiga mkono wake wa kulia kwa kumshutikiza kisu kikaangukia mbali, akawekwa chini ya ulinzi. Kumbe kile kisu mbali na kumuua mkewe alikitumia kujaribu kujichinja koo lakini ikashindikana,” alisema mhudumu huyo.

Mwanaume akiwa chini ya ulinzi na pingu mikononi, polisi waliingia chumbani na kukuta damu kila mahali. Cha kusikitisha zaidi, mwili wa marehemu Josephine ulipigishwa magoti, sehemu ya miguu mpaka magoti ikiwa sakafuni na kifuani kulalia kitanda. 
 
Halafu ulifunikwa shuka.“Kwa mbali ungeweza kusema kuna binadamu anasali kwa namna ambavyo marehemu huyo alivyokuwa amepigishwa magoti,” alisema mhudumu huyo.

Katika hali iliyoonesha kuwa, mtuhumiwa baada ya kutenda ukatili huo alitaka kujinyonga, polisi walikuta waya wa umeme wa tivii ukining’inia kwenye pangaboi lakini ukiwa umekatika.

Polisi walifanya uchunguzi chumbani na kugundua kuwa, marehemu Josephine alichinjwa shingoni, akakatwa mbavu mbili, moyo na maini vilikuwa nje ‘vikimwagika’, mwisho alichomwa kisu utosini.

Pia kwenye chumba hicho, polisi walikuta simu mbili, ya marehemu na ya mtuhumiwa zikiwa zimeharibiwa laini kiasi cha kukosa mawasiliano.

Mwandishi alipata bahati ya kuzungumza na mtuhumiwa huyo kabla ya kupelekwa Kituo cha Polisi Magomeni, Dar ambapo alisema Josephine alikuwa mke wake na wameishi kwa muda zaidi ya miaka kumi na kupata watoto wawili. Hata hivyo, hakuongea zaidi ya hapo.

Msimamizi mkuu wa hoteli hiyo aliyejitambulisha kwa jina la Zuberi Hussein alipohojiwa  alisema:

“Tuliwapokea hawa watu kama wateja wengine. Walilipa shilingi elfu kumi na tano kwa chumba.  Hatukujua kama haya yangetokea, wahudumu ndiyo walibaini baada ya kuona damu ikitiririka mlangoni.”

Baadaye, polisi waliupakiza mwili wa marehemu kwenye gari kuupeleka Hospitali ya Taifa Muhimbili huku mtuhumiwa akipelekwa Kituo cha Polisi Magomeni jijini Dar pembeni yake akiwa amelala marehemu mkewe.

Baada ya hapo,Mwandishi wetu alifunga safari hadi eneo la Studio, Kinondoni, Dar nyumbani kwa David Ndeshao Mushi ambaye ni kaka wa marehemu na ndiko sehemu ulipowekwa msiba.

Baadhi ya ndugu wa marehemu walidai kwamba, Josephine na mumewe mara kwa mara walikuwa na migogoro  ya ndoa.

“Ndoa yao haikutulia, walikuwa wanapatanishwa lakini baada ya muda mfupi wanaanza tena ugomvi. Mumewe alikuwa akimhisi vibaya mke wake. Hata hivyo, Desemba mwaka jana, Josephine alienda kuishi kwa kaka yake kutokana na ugomvi,”alisema mmoja wa wanandugu wa karibu.

Kaka mtu  huyo alipohojiwa alisema: “Marehemu alirudi kwangu lakini tulikuwa hatujaongea naye kuhusu ugomvi wao. Nilisafiri mkoani nikamuacha, niliporudi, Jumatano alienda kazini lakini hakurudi. Tulipopiga simu yake akawa hapatikani. Mumewe naye akawa hapatikani hadi taarifa ilipotufikia kwamba kauawa hotelini.

“Tunatarajia kusafirisha mwili kwenda Moshi, Jumapili (juzi). Mazishi yatakuwa Jumatatu (jana). Marehemu ameacha watoto wawili ambao walikuwa wakiishi Tabata, Dar.”

Inadaiwa kuwa, mtuhumiwa alikuwa mfanyakazi wa Baa ya Break Point iliyopo jijini Dar. Marehemu alikuwa mfanyakazi katika Kampuni ya TAC iliyopo Upanga, Dar.

Mmoja wa marafiki zake wa karibu alisema Jumatano mchana, mumewe alimfuata kazini na wakawa na mazungumzo, alimtaka waondoke lakini marehemu alikataa.Alimbembeleza sana mwishowe wakakubaliana na kuondoka lakini wakashangaa kusikia alimuua hotelini.


Comments

Popular posts from this blog

JINSI YA KUKAA NA NGUVU ZA MUNGU SEHEMU YA KWANZA

MAGONJWA 27 YANAYOTIBIWA NA ASALI YENYE MDALASINI