KITIMTIM BUNGENI



          Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akizungumza bungeni Dodoma jana. 

Dodoma. Kitimtim bungeni. Hicho ndicho kilichotokea bungeni jana baada ya Naibu Spika, Job Ndugai kuwaomba wabunge kukishauri kiti chake juu ya hatua ya kuwasilishwa na kujadiliwa kwa ripoti ya uchunguzi wa IPTL kwa madai ya kuwapo kesi mahakamani.
Wabunge wa pande zote – chama tawala na upinzani  waliopata fursa ya kuzungumza, walitoa kauli zinazofanana za kutaka suala hilo lijadiliwe na chombo hicho cha kutunga sheria, huku wakipinga njama za kutaka kuzima hoja.
Hata pale Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alipojaribu kueleza umuhimu wa kumaliza suala hilo bila mihimili ya Bunge na Mahakama kuingiliana, zilisikika sauti wabunge wakimzomea, ikimaanisha kuwa suala hilo lazima lijadiliwe kwa uwazi bungeni.
Kwa jinsi mjadala huo wa wabunge ulivyokwenda, ni dhahiri kwamba ripoti hiyo iliyochunguza kuchotwa kwa Sh306 bilioni katika akaunti ya Tegeta Escrow italeta mtikisiko mkubwa serikalini na bungeni kama ambavyo gazeti hili liliripoti Jumanne iliyopita.
Wabunge wanane waliochangia mjadala huo walionekana wazi kutaka kiti cha Spika kitumie mamlaka yake vizuri kuhakikisha ripoti hiyo inawasilishwa bungeni haraka na kujadiliwa ili waliochota fedha hizo “wabebe msalaba wao”.
Mjadala huo mkali uliibuka baada ya kuibuka taarifa kwamba kuna barua kutoka mahakamani iliyowasilishwa kwa Bunge kutaka kuzuiwa kwa mjadala huo, barua ambayo hata hivyo, Ndugai alisema hajaiona.
Naibu Spika alitoa fursa hiyo baada ya kuombwa mwongozo na Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila aliyetaka kujua iwapo ripoti hiyo itawasilishwa bungeni au la, kutokana na kuwapo kwa madai ya barua kutoka mahakamani.
“Tunataka tujue ripoti italetwa au la, tunasikia kuna mkakati wa kimahakama kuzuia isije, sasa tunataka utuhakikishie kama itaingia bungeni kwa kuwa Mahakama haipaswi kuingilia Bunge,” alisema Kafulila.
Kabla ya kujibu mwongozo huo, Ndugai alisema: “Kama mlivyozungumza hili ni jambo la haki za Bunge, sasa naomba mkisaidie kiti tujadili mwelekeo.”
Kafulila
Aliyepewa nafasi ya kufungua mjadala huo ni Kafulila aliyeanza kwa kutoa ushauri kwa kiti cha Spika kuwa Bunge ndilo lenye mamlaka ya mwisho na wabunge ndiyo wawakilishi wa wananchi, hivyo kuna mtihani kuhusu jambo hilo na Bunge ndilo litaamua.
“Ni lazima tujue kama Bunge tunatosha au hatutoshi, kama Bunge linaweza au haliwezi. Kama taarifa zinasema kuna majaji na viongozi wamekula fedha hizo halafu kuna hoja ya kuzuia eti jambo liko mahakamani. Hilo jambo halina msingi kama kweli kuna hoja ya Mahakama mbona CAG alipochunguza kwa niaba ya Bunge haikuzuia?”

Comments

Popular posts from this blog

JINSI YA KUKAA NA NGUVU ZA MUNGU SEHEMU YA KWANZA

MAGONJWA 27 YANAYOTIBIWA NA ASALI YENYE MDALASINI