LIPUMBA; CCM ING'OKE KWANZA RUZUKU BAADAE




                       Mwenyekiti wa CUF Prof. Ibrahim Lipumba

Wakati Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi akisema suala la ruzuku na viti maalumu ni changamoto kwa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba amesema hicho si kipaumbele.
“Tunachokitaka ni kuunganisha nguvu zetu ili kuhakikisha tunaing’oa CCM madarakani kwanza, masuala mengine kuhusu ruzuku tutaweka utaratibu maalumu baadaye,” alisema.
Profesa Lipumba ambaye pia ni mwenyekiti mwenza wa Ukawa, alisema hayo Dar es Salaam jana alipokuwa akiwaeleza waandishi wa habari maazimio ya Baraza Kuu la Uongozi la Taifa la CUF lililokutana Jumatatu na Jumanne iliyopita.
“Wenzetu Kenya waliweza kuungana na kuhakikisha wanaking’oa chama tawala madarakani, lakini sasa kwa hapa mkiungana na kuwa chama kimoja ni lazima msajili chama chenu, sasa tunachokitaka ni kushirikiana tu kwanza,’’ alisema.
Alisema suala la ruzuku na uteuzi wa viti maalumu siyo lengo kuu la Ukawa inayoundwa na vyama vinne; CUF, Chadema, NCCR-Mageuzi na NLD kwa kuwa linajadilika. Alisema jambo la msingi hivi sasa ni ushirikiano wa amani.
Alisema kinachotakiwa kwa viongozi wa Ukawa ni kuaminiana kwanza ili kulinda muungano huo ambao alisema umeshaanza kukitikisa chama tawala, CCM.
Maazimio ya Baraza Kuu
Alisema Baraza hilo lilisisitiza umuhimu wa kuaminiana miongoni mwa vyama washirika katika ngazi zote ili kudumisha umoja huo na kufikia lengo la kuitoa CCM madarakani.
“Baraza limetaka uwepo utaratibu mzuri na wa wazi utakaoonyesha mambo ya msingi ambayo vyama vinavyounda Ukawa vimekubaliana. Utaratibu huu uwafikie viongozi wa ngazi zote za chama ili kuhakikisha jukwaa la Ukawa linatumika kwa lengo na dhamira iliyopo ndani ya hati ya makubaliano ambayo ni kuing’oa CCM madarakani,” alisema.
Kuhusu uchaguzi wa Serikali za Mitaa Profesa Lipumba alisema Baraza limetaka sheria irekebishwe ili uchaguzi wa diwani ufanyike pamoja na wa viongozi wa mitaa, vijiji na vitongoji kwa wakati mmoja, kwa vile diwani ndiye kiongozi mkuu wa kuchaguliwa wa kata.
Baraza hilo pia limetaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), iratibu na kusimamia uchaguzi wa Serikali za Mitaa na utengenezwe utaratibu ambao utaifanya Tume hiyo kuwa huru kuwezesha chaguzi zote zijazo kufanyika kwa uhuru na haki.
“Taarifa za Tume zilieleza kuwa itaandikisha wapigakura mpaka kwenye ngazi ya vijiji na vitongoji, kwa hiyo uchaguzi wa Serikali za Mitaa usubiri mpaka daftari la kudumu la wapigakura likamilike na ndilo litumiwe kwenye uchaguzi huo,” alisema.

Comments

Popular posts from this blog

JINSI YA KUKAA NA NGUVU ZA MUNGU SEHEMU YA KWANZA

MAGONJWA 27 YANAYOTIBIWA NA ASALI YENYE MDALASINI