MUME AMCHARANGA MAPANGA MKEWE KISA KACHELEWA USHIKA UJAUZITO


Mtu mmoja mwanamume, aliyetajwa kwa jina la John Weghai amemjeruhi vibaya mke wake, Anastazia John (18) kwa kumkatakata na mapanga kwa kile kinachodaiwa kuchelewa kwake kupata ujauzito, katika maisha ya wawili hao waliyoanza Februari mwaka jana.

Tukio hilo la kinyama lilitokea katika Kijiji cha Mariba, Kata ya Mriba, wilayani Tarime mkoani Mara na majeruhi huyo amelazwa katika hospitali ya Halmashauri ya Mji ambapo ameshonwa nyuzi 67.
 
Akizungumzia tukio hilo, msichana huyo alisema kuwa mumewe amekuwa akimpa matatizo mengi katika ndoa yake kiasi cha kumkosesha amani kwa kumpiga mara kwa mara akimtuhumu kuchelewa kupata ujauzito.
 
“Kwa kweli nimekuwa nikipata mateso makubwa tangu niishi na mwanaume huyu, nimekuwa nikipigwa mara kwa mara sababu nachelewa kupata mimba na yeye anataka mtoto.
 
“Naviomba vyombo vinavyotetea na kusaidia matatizo ya ukatili kama haya viweze kusaidia watu wanaofanyiwa maana yanaondoa utu wa mtu na kumfanya kuishi kinyonge,”alisema Anastazia.
 
Alisema siku hiyo alipata majeraha makubwa katika bega na titi lake la kushoto, kitu kinachompatia maumivu makubwa.
 
Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (Tamwa), Valeria Msoka, alisema wamesikitishwa na tukio hilo, akisema ni ukatili uliopitiliza lakini wataendelea na jitihada za kupambana na matukio ya namna hiyo katika jamii.
 
Alisema muda mfupi tu umepita tokea warejee kutoka wilayani Tarime wakiwa na ugeni mkubwa wa kimataifa kupambana na masuala ya ukatili na kutoa ujumbe kwa wananchi juu ya athari zake lakini kuna watu hawajabadilika.

“Tulitoa maoni kwenye Katiba mpya inayopendekezwa na tunashukuru yamepita juu ya kuangaliwa upya kwa sheria ya wanaofanya makosa ya ukatili kwenye jamii huenda ikaja kuwa suluhisho juu ya matukio haya,”alisema Msoka.
 
Kufuatia tukio hilo, Jeshi la Polisi Kanda maalum ya kipolisi Tarime/Rorya limesema mtuhumiwa bado hajakamatwa na jitihada za kina zinaendelea kufanywa ili kuhakikisha anakamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.
 
Kaimu Kamanda wa Tarime/Rorya, Sweetbet Njwewike alisema katika tukio hilo lililotokea Januari 22 mwaka huu lilichelewa kutolewa taarifa jambo ambalo limechelewesha kupatikana kwa mtuhumiwa.
 
Tukio hilo limetokea siku chache tu tokea mke wa Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, Graca Machel kuwepo wilayani Tarime, akihamasisha kampeni ya kuepuka ukatili kwa watoto na akina mama

Comments

Popular posts from this blog

JINSI YA KUKAA NA NGUVU ZA MUNGU SEHEMU YA KWANZA

MAGONJWA 27 YANAYOTIBIWA NA ASALI YENYE MDALASINI