MJAMZITO AJIFUNGULIA BAFUNI DAKIKA CHACHE BAADA YA WAUGUZI KUMFUKUZA



MJAMZITO aliyefahamika kwa jina la Rotha Bujiku, amejifungulia bafuni karibu na zahanati ya kijiji baada ya kudaiwa kufukuzwa na wauguzi waliokuwa zamu siku hiyo, kwa maelezo kuwa anajifungua kila mwaka.
 
Tukio hilo lilitokea wilaya ya Maswa katika mkoa wa Simiyu majira ya saa 2 asubuhi baada ya mjamzito huyo kufika katika zahanati hiyo kwa lengo la kupata huduma ya kujifungulia kwa wataalamu.
 
Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo lililovuta umati wa watu, mjamzito huyo alikataliwa kupokewa na muuguzi wa zamu aliyetajwa kwa jina la Constansia John.
 
Ilielezwa kuwa muuguzi huyo alikataa kumpokea kwa madai kuwa mjamzito huyo alishapewa maelekezo tangu awali kuwa anatakiwa akajifungue katika hospitali ya wilaya ya Maswa kwani amekuwa akizaa watoto kwa mfululizo.
 
Inaelezwa kwamba, wakati Rotha akiugulia maumivu ya uchungu, muuguzi huyo alimpigia simu ya mkononi Muuguzi Mkunga wa zahanati hiyo, Leticia Kachumi kumjulisha hali hiyo na alipofika alitaka mjamzito huyo aondoke katika eneo hilo na atafute usafiri ili aweze kufika katika hospitali ya wilaya kama alivyoelekezwa katika siku za nyuma.
 
“Leticia alipofika hapo zahanati baada ya kupigiwa simu na Constansia, licha ya kumuona anaendelea kulalamika kutokana na uchungu alimwamuru aondoke eneo hilo mara moja na atafute usafiri wa kumfikisha hospitali ya wilaya iliyoko umbali wa kilomita 36, kwani walishamweleza kuwa amekuwa akizaa mfululizo na hiyo ni mimba ya kumi na moja,” alisema shuhuda, Kundi Mageni.
 
Kutokana na hali hiyo, mjamzito huyo alilazimika kuondoka zahanati hapo bila msaada wowote na baada kufika karibu na nyumba iliyoko na zahanati hiyo, alikwenda katika bafu la nyumba ya jirani ambalo halina sakafu na kujifungulia humo na baadaye kusaidiwa na wasamaria wema waliosikia sauti ya mtoto.
 
“Kwa kweli huyu mama amejifungulia katika mazingira machafu na hatarishi kwa afya yake na mtoto aliyemzaa. Kwa kweli hili ni tukio la kusikitisha. Huwezi kuamini wauuguzi hao ambao ni wanawake kumtendea mwenzao ukatili wa kiasi hiki,” alisema Pili Kidesela, Diwani wa kata ya Shishiyu (CCM).
 
Mganga Mkuu wa Wilaya ya Maswa, Dk Jonathan Budenu aliyefika katika eneo la tukio muda mfupi baada ya kupata taarifa hizo, alisema kitendo kilichofanywa na wauguzi hao ni kinyume cha maadili ya kazi yao na hivyo ni lazima hatua kali za kinidhamu zichukuliwe kwa wote waliohusika.
 
Mwingine ajifungulia kichakani 
Wakati hayo yakitokea Maswa, mkoani Arusha binti mwenye umri wa miaka 17 alijikuta akijifungulia kichakani baada ya kuzidiwa uchungu wakati akisubiri kuombewa kwenye mkutano wa dini uliofanyika Viwanja vya Magereza, Kisongo nje kidogo na Jiji la Arusha.
 
Anna Ngitoria, mkazi wa Endurimeti, wilayani Arumeru, alikuwa miongoni mwa mamia ya wakazi wa Arusha, Kilimanjaro na vitongoji vyake waliokuwa wamekusanyika kwa wingi kwenye uwanja huo wa magereza kwa ajili ya kile kilichodaiwa kuwa ni maombi yaliyoandaliwa na kituo kimoja cha redio cha jijini Arusha, Radio Safina.
 
Kwa kawaida uongozi wa kituo hicho huandaa makongamano ya kila mwezi kwenye uwanja huo wa Kisongo na kujumuisha mamia ya watu, wengi wao wakiwa ni wanawake na wasichana ambao hupendelea kuhudhuria maombezi hayo kwa matarajio tofauti.
 
Mikusanyiko ya maombi ya ‘Radio Safina’ imekuwa ikikusanya watu wengi mithili ya ‘Kikombe cha Babu,’ ambacho nacho kilivuma sana miaka mitatu iliyopita na tukio la msichana huyo kujifungua katika moja ya matukio hayo kimezua hisia tofauti mjini hapa.
 
Akizungumza katika hospitali ya Mount Meru ambapo amelazwa kwa sasa, binti huyo, Anna amekiri kuwa alijifungua kabla ya wakati kwa sababu alikuwa na ujauzito wa miezi saba tu.
 
Mtoto wake njiti sasa anahudumiwa katika wodi maalumu iliyopo hospitalini hapo na wauguzi wanasema anaendelea vizuri.

Comments

Popular posts from this blog

JINSI YA KUKAA NA NGUVU ZA MUNGU SEHEMU YA KWANZA