MTOTO WA MIEZI MITATU AATHIRIKA NA DAWA ZA KULEVYA



                           Zena akiwa na mtoto wake
Dar es Salaam. Mtoto mwenye umri wa miezi mitatu, mkazi wa Buza, Dar es Salaam amebainika kuwa mwathirika wa dawa za kulevya.
Damu na mkojo vya mtoto huyo (jina tunalihifadhi) vilichukuliwa na kupimwa katika maabara ya Hospitali ya Mwananyamala na baada ya saa mbili, majibu yalitoka na kuthibitisha kwamba alikuwa na chembechembe za dawa za kulevya aina ya heroini.
Taarifa za kitabibu zinaonyesha kuwa kuwapo kwa heroini mwilini mwa mtu, huweza kuonekana katika mkojo ndani ya siku mbili hadi nne iwapo dawa hizo zilitumiwa na mhusika kwa kati ya saa mbili hadi tano.
Hatua ya kumfanyia vipimo mtoto huyo wa kiume, inatokana na jitihada za gazeti hili kutaka kufahamu jinsi utumiaji wa dawa za kulevya kwa wanawake wajawazito na wale wanaonyonyesha unavyoweza kumwathiri mtoto akiwa tumboni au anayenyonya maziwa ya mama mwathirika.
Mtaalamu wa tiba katika Hospitali ya Mwananyamala, Dk Elifasi Mritu anasema: “Ni kweli ukitumia dawa za kulevya wakati unanyonyesha au wakati wa mimba, mtoto naye huathirika.”
Kauli ya Dk Mritu ambaye ni daktari katika kitengo cha tiba ya methadone hospitalini hapo, inaungwa mkono na Mkuu wa Kitengo cha Magonjwa ya Akili katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dk Frank Mushi ambaye anasema mama anayetumia dawa za kulevya akiwa mjamzito humwathiri pia mtoto.
Mama wa mtoto azungumza
Mama wa mtoto, Zena maarufu Zerish, mkazi wa Yombo Buza alikiri kwamba alipata ujauzito wakati akitumia dawa za kulevya na kwamba hadi sasa anavuta dawa hizo huku akiendelea kumnyonyesha mtoto huyo.
Anasema baada ya kujifungua hakukaa ndani kwa siku 40 kama wafanyavyo wanawake wengi wa Kitanzania, kwa sababu mwili wake ulikuwa unahitaji ‘unga’ vinginevyo hali yake huwa mbaya.
Anasema baada ya kujifungua alianza kuzunguka huku na kule akiwa na mtoto mgongoni, huku akiwa amebeba mfuko wake wa plastiki wenye mahitaji muhimu ya mtoto kama nepi na nguo.
Anasema anapovuta au kujichoma dawa, mtoto wake pia hupata ‘stimu’ kwa sababu hupata dawa hizo za kulevya kupitia maziwa anayonyonya na hivyo wote wawili kulala fofofo sehemu yoyote ile.
Hata hivyo, kwa Zerish na mwanaye, anapofikia hali ya kuwa ‘alosto’ (wakati dawa za kulevya zinapoisha mwilini na hivyo kuhitaji tena), huwa ni adhabu kali mno.

Comments

Popular posts from this blog

JINSI YA KUKAA NA NGUVU ZA MUNGU SEHEMU YA KWANZA

MAGONJWA 27 YANAYOTIBIWA NA ASALI YENYE MDALASINI