KINGUNGE AENDELEA KUMLILIA LOWASSA, ASEMA SIO FISADI KAMA ANAVYOSEMWA



Mwanasiasa Mkongwe katika medani za siasa nchini Tanzania Kingunge Ngombale Mwiru ameibuka na kuzungumza na Waandishi wa Habari leo  kuhusiana na  mchakato wa kumpata mgombea Urais CCM uliopelekea jina la Mbunge wa Monduli Edward Lowassa kukatwa.

Akizungumza katika mkutano huo Kingunge amesema   Kamati ya Maadili huko nyuma ilikuwa ni chombo cha kuandaa taarifa ili kuisadia Kamati Kuu katika  kuwajadili wagombea  lakini safari hii Kamati ya Maadili imefanya kazi isiyowahusu kikatiba  ikiwemo  kukata majina ya wagombea.

Amesema  Kamati ya Maadili ya Chama cha Mapinduzi (CCM)  yenyewe imekosa maadili ya kuheshimu katiba na taratibu za chama kwa kujipa madaraka ya kupeleka majina 5 kwenye kamati kuu, ambayo ilipaswa kuhoji wagombea wote 38.

“Kuna baadhi ya watu waliamua kuitumia Kamati ya Maadili kuandaa watu wao na kuwakata wengine kwa sababu zao.” Amesema Kingunge.

Kingunge  amedai kwamba  CCM ni chama cha wanachama wote, taratibu na kanuni zikipuuzwa na kufanya vitu kwa maamuzi ya kikundi fulani, amedai kuwa  kwenye vikao vya CCM Ulifanyika uhuni na dharau kwa wanachama wengine.

"Wakubwa waliopewa madaraka wanaona hakuna lolote tunaloweza kufanya."

Amesisitiza kuwa kilichofanyika Dodoma hakikuwa sawa, Kamati Kuu iliporwa kazi yake, hii ni dharau kwa wanachama na wagombea wote. Kamati Kuu ya Taifa CCM, ipo chini ya Halmshauri Kuu ya Taifa yenye madaraka ya kujadili mapendekezo yalioletwa na Kamati Kuu,  na Halmshauri Kuu ina madaraka ya kukataa au kukubali mapendekezo yalioletwa na Kamati Kuu, lakini utaratibu huo haukuwepo

Kingunge amesema  anawaheshimu sana Mzee  Benjamin  Mkapa, Mwinyi, na Karume, lakini amesikitika kuwa  ndio  waliotoa  michango  ya  kutotoa  haki kwenye Kamati Kuu.
  
"Waliogombea 1995 walikuwa 16, Kamati Kuu iliwasikiliza na kuandaa orodha ya watu 6,” alisema Kingunge.

Akizungumzia yaliyokea NEC Kingunge amesema wajumbe walihoji kwa nini  Jina La Lowassa halikuwemo, mjadala ulikuwa mgumu, watu walisema lazima aingie kwenye orodha. "......Kwa mara ya kwanza muundo wa Chama ulijaribiwa baada ya wajumbe kutaka jina la Lowassa kwenye orodha ya majina 5."

Kwa upande mwingine, amewapongeza wajumbe walijitokeza kukataa  maamuzi ya Kamati Kuu ikiwemo  Adam Kimbisa, Mbunge wa Songea Emmanuel  Nchimbi na Sophia Simba.

Akizungumzia kauli ya Mbunge huyo kuhusishwa na ufisadi Kingunge amesema,
 
"Hadithi ya Lowassa kuwa ni fisadi haina mashiko, ilianza kwa kashfa ya Richmond. Kamati teule ya Bunge iliundwa na kutoa taarifa za ovyo sana, na hatimaye kwa kulinda heshima ya serikali na chama akajiuzulu."

Kingunge  ameongeza kuwa  Lowassa sio wa kwanza kuwajibika kisiasa .Amesema katika  awamu ya kwanza ya Mwalimu –walikuwemo   viongozi wa kisiasa waliouzulu.
  
Amewataja waliowahi kujiuzulu  kuwa   ni Waziri wa Mambo ya Ndani,  Ali Hassani Mwinyi, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga na Mkurugenzi wa Usalama Taifa wote walijiuzulu kisiasa na Mwalimu aliwashukuru kwa kuwajibika.

“Lowassa alijiuzulu kuwajibika kisiasa, lakini ikabadilishwa kuonekana ni yeye ndiye aliyefanya makosa, ndio ukaanza wimbo wa ufisadi. Serikali yenyewe ilimsafisha kupitia TAKUKURU, lakini wimbo wa ufisadi ukaendelea, wakaja na wimbo mwingine wa Gamba.

“Yote haya yalipangwa na ‘Kitengo’ kilichoandaa kashfa ya Richmond. Edward ana historia ndefu ndani ya Chama.” amesema  mzee Kingunge.

Amesisitiza kuwa  Uongozi wa Chama na Nchi umetumia nguvu kubwa sana kupuuza wananchi wanataka nini na kuhakikisha wanayempenda hapati kitu

Ametumia mkutano huo pia kuwaomba viongozi ndani ya CCM warudi kusoma ahadi za mwanachama, warudi pia wasome utangulizi wa katiba ya CCM na kusisitiza kuwa  kilichotokea Dodoma hakikubaliki, si halali na si haki.

Comments

Popular posts from this blog

JINSI YA KUKAA NA NGUVU ZA MUNGU SEHEMU YA KWANZA