HOTUBA YA MH. ZITTO KABWE KUHUSU HALI YA NCHI KATIKA MKUTANO WA KIDEMOKRASIA WA ACT WAZALENDO
Ndugu Mama Anna Elisha Mghwira, Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha Wazalendo, Ndugu Viongozi wote wa chama katika ngazi mbalimbali Ndugu Wanachama Ndugu wageni waalikwa Ndugu wananchi Mabibi na Mabwana Karibuni Sana! Ninayo furaha na heshima kubwa kusimama mbele yenu na kuhutubia kwa mara ya kwanza katika Mkutano wa Kwanza wa Kidemokrasia wa Chama chetu. Mkutano wa kidemokrasia ni kikao pekee rasmi cha kikatiba katika chama chetu ambapo viongozi na wanachama wanakutana ana kwa ana na kubadilisha mawazo kuhusu chama na maendeleo ya nchi yetu kwa ujumla. Aidha, katika mkutano huu tunawaalika wageni mbalimbali kutoka nchi na vyama marafiki kwa ajili ya kubadilisha uzoefu katika nyanja mbalimbali. Mkutano wa Kidemokrasia ni kikao cha aina yake kwa kuwa wanachama na waalikwa wengine wanahudhuria kwa hiari yao na kwa gharama zao. Muhimu zaidi ni kwamba katika kikao hiki hata wananchi wasio wanachama wanakaribishwa kuhudhuria ili wasikilize na kushiriki kutoa maoni ...